| SALAMU
ZA MKURUGENZI MKUU KWA WAFANYAKAZI WOTE WA MAMLAKA YA VIWANJA
VYA NDEGE KWA KUMALIZA MWAKA 2004 NA KUANZA
MWAKA MPYA WA 2005.
Ndugu Wakurugenzi, Wakuu wa
Vitengo, Mameneja, Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi na
Wafanyakazi wote - Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania.
Kwa niaba ya Uongozi wa Mamlaka
ya Viwanja vya Ndege Tanzania na kwa niaba yangu binafsi,
nachukua fursa hii fupi kuwapeni pongezi kwa kumaliza mwaka wa
2004 na kuanza mwaka mpya wa 2005.
Ni matumaini yangu kuwa kila
mmoja wetu anayo furaha isiyopimika kwa kubarikiwa nafasi hii
ya pekee.
Hivyo basi sote hatuna budi
kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema zake alizotujalia na
kutufikisha hapa tulipo.
Katika kuifurahia nafasi hii
ni vema kukumbuka na kutafakari kwa makini ili kuona ni mambo
yapi tulitarajia kuyafanya kwa kipindi cha mwaka tunaoumaliza na
kwa kiwango gani tumetekeleza au tumefikia katika utekelezaji
wake, au kukwama na kuchambua changamoto zilizotukabili katika
utendaji wa kazi zetu.
Kwa kufanya hivyo tunajiweka
katika nafasi ya kujua wapi tulipofika, na misingi
iliyotufikisha hapo.
Tukiwa tumejua mahali tulipo,
ni wajibu wetu kutazama mbele ili kuona ni mahali gani
tunatarajia kufika katika kipindi kinachofuata na kutambua mambo
ambayo tunapaswa kuyafanya, hasa tukitilia maanani kukidhi
mahitaji ya wanaotumia huduma zetu na hivyo kufikia malengo
tuliyojiwekea.
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege
Tanzania kama mdau katika sekta ya usafiri wa anga ina malengo
na majukumu ambayo ni changamoto kubwa kwa Mamlaka yenyewe,
Taifa na Ulimwengu kwa ujumla.
Changamoto hizi zinatokana na
mfumo mzima wa mabadiliko yanayotokea ulimwenguni hususan katika
sayansi na teknolojia. Sekta ya usafiri wa anga ni moja ya
maeneo ambayo yameendelea na mabadiliko makubwa na ya haraka
ambayo yanahitaji kufuatiliwa kwa karibu ili kuweza kuhimili
ushindani katika utoaji huduma kwa misingi ya biashara.
Katika salamu zangu nilizotoa
mwaka jana, nilieleza baadhi ya mambo ambayo Mamlaka yetu
ilikuwa inakabiliana nayo kama changamoto; hii ikiwa ni pamoja
na :
* Uhaba/upungufu
wa fedha kutokana na uchache wa vyanzo vya mapato ikilinganishwa
na mahitaji makubwa ya ukarabati, ujenzi na uboreshaji wa miundo
mbinu ya viwanja vya ndege.
* Hali
isiyoridhisha ya Viwanja vyetu vya Ndege hususan uchakavu na
upungufu wa vifaa na miundo mbinu.
* Kuendelea kwa
vitendo vya ugaidi kuwa tishio kwa maangamizi ya mali na maisha
ya watu katika sekta nzima ya usafiri wa anga.
* Janga la
Ukimwi ambalo linaendelea kuwa tishio la “nguvu kazi” katika
utendaji wa shughuli za Mamlaka na Taifa kwa ujumla.
Napenda nitamke wazi kuwa mambo
haya bado ni changamoto kubwa hadi leo na bado juhudi za pamoja
zinahitajika ili kuendelea kukabiliana nayo katika kipindi
kinachofuata.
Hata hivyo, kwa niaba ya
Uongozi wa Mamlaka , nawajibika kutoa shukrani za dhati kuwa
katika kipindi cha mwaka 2004, tumekuwa na maelewano ya Kiwango
cha juu kati ya viongozi na watumishi katika sehemu mbalimbali
za kazi katika kukabili changamoto hizo.
Wafanyakazi wote kwa pamoja na
kila mmoja kwa nafasi yake mmeonesha uwezo na ushirikiano mkubwa
wa kiutendaji. Hali hii imebainisha kujengeka na kukua kwa umoja
na kutambua umuhimu wa mshikamano miongoni mwetu katika utendaji
wa majukumu tuliyokabidhiwa. Napenda niwashukuru sana kwa hili
na kuwaomba tuongeze juhudi za kudumisha umoja wetu.
Katika mwaka tunaomaliza wa
2004, tulitarajia kufanya yafuatayo ikiwa ni sehemu tu ya mambo
mengi :-
(i) Kukamilisha taratibu za uhamisho wa moja kwa moja wa
wafanyakazi. Matarajio
yalikuwa suala hili
likamilike ndani ya miezi mitatu (3) ya kwanza ya mwaka
2004.
·
Nashukuru kwamba
suala hili lilikamilika na hivyo kuondoa hofu iliyokuwa
imewagusa watumishi kuhusu hatima ya utumishi wao.
(ii) Kuimarisha
ushirikishwaji wa Wafanyakazi katika maamuzi na mipango ya
Mamlaka kupitia Baraza la Wafanyakazi.
·
Kufuatia kuundwa
kwake mwezi Novemba 2003, baraza la Wafanyakazi limekuwa chombo
muhimu kinachosaidia Uongozi wa Mamlaka katika kufanya maamuzi
ya kiuendeshaji. Katika kipindi cha mwaka 2004, Baraza lilifanya
vikao viwili kwa mujibu wa Mkataba.
(iii) Kuendelea
kukamilisha taratibu za ajira kujaza nafasi zilizokuwa wazi kwa
kuzingatia mahitaji ya kazi, kadiri itakavyojitokeza.
·
Taratibu za ajira
ziliendelea kufanyika kwa kuzingatia umuhimu ili kujaza nafasi
zilizo kuwa wazi na hivyo kupunguza uzito wa kazi kwa watumishi
wengine.
(iv) Kukamilisha taratibu
za upimaji wa wazi wa utendaji kazi (OPEN PERFORMANCE
REVIEW AND APPRAISAL
SYSTEM – OPRAS) kuanzia Julai 1, 2004.
·
Kutokana na
sababu zisizozuilika, lengo hili halikufikiwa kama ilivyokuwa
imekusudiwa. Hata hivyo, nashukuru kwamba kwa kiasi kikubwa
baadhi yenu pamoja na kutopewa mafunzo, wamefanya juhudi za
kutengeneza mikataba ya utendaji (Performance Agreement)
na kuisaini. Natumaini kuwa mikataba hiyo itaendelea kuwa
miongozo katika utendaji kazi za kila siku na hatimaye kutumika
katika upimaji wa utendaji kazi.
(v) Kuimarisha na
kuboresha utendaji wa kazi kwa kutoa mafunzo yanayolenga
kuongeza uwezo wa
mtumishi kufanya kazi zake kwa umakini na ufanisi zaidi.
·
Juhudi za kutoa
mafunzo kwa watumishi ziliendelea, hii ikiwa ni pamoja na
kutayarisha Mpango wa Mafunzo (Training Program). Hata hivyo
kutokana na hali isiyoridhisha ya uwezo wa kifedha wa Mamlaka,
utoaji wa mafunzo ulielekezwa kuwawezesha watumishi
kuongeza uwezo wa kufanya kazi kwa umakini na ufanisi zaidi.
(vi) Kuendelea na ujenzi wa
kiwanja cha Ndege cha Songwe - Mbeya.
·
Ujenzi wa Kiwanja
cha ndege cha Songwe uliendelea kwa kasi ya kuridhisha.
(vii) Kuendelea na ukarabati wa
mfumo wa umeme kwenye kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha
Dar es Salaam ambao ulitarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa
mwaka 2004.
·
Kazi ya ukarabati
wa mfumo wa umeme iliendelea vizuri na ilikamilika mwezi Mei
2004 (kabla ya muda uliokuwa umetarajiwa).
(viii) Kuendelea na juhudi
za kuimarisha hali ya usalama (safety and Security)
kwenye viwanja vya ndege kulingana na viwango vya ICAO.
·
Pamoja na kutoa
mafunzo yanayohusika, utekelezaji wa "Airport Security
Programme na Airport Emergency Plan" kila
kiwanja, Mamlaka iliendelea na juhudi za kutoa vifaa
vinavyohusika na kujenga uzio kwa kuzingatia uwezo wa kifedha wa
Mamlaka na kutoa kipaumbele kwa maeneo hayo mawili yaani
"safety & security". Kitengo kipya cha “Compliance”
kimeanzishwa kulingana na muundo wa Mamlaka, kwa ajili ya
uthibiti wa ndani ili kujihakikishia kuwa tunakidhi viwango vya
ICAO vya “Safety & Security” kabla ya ukaguzi.
(ix)
Kuendelea na juhudi za kutafuta vyanzo vipya vya mapato
na kuboresha vile vilivyopo ili kuendelea kujenga
uwezo wa Mamlaka kifedha.
·
Mamlaka
iliendelea na juhudi za kutafuta vyanzo vipya vya mapato na
kuboresha vile vilivyopo ili kuendelea kujenga uwezo wa Mamlaka
kifedha; hii ikiwa ni pamoja na kuweka misingi ya kushirikisha
sekta binafsi katika uwekezaji kwenye viwanja vyetu vya ndege.
(x) Kuendelea
kushirikiana na wadau katika kuanzisha maeneo huru ya
utengenezaji na usafirishaji bidhaa nje ya nchi (Export
Processing Zone) kwenye Viwanja vya Ndege hususan DIA.
·
Kutokana na
sababu zisizozuilika, Mamlaka haikuweza kufanikiwa sana katika
suala hili. Bado juhudi zinaendelea kulifanyia kazi zaidi.
(xi) Kukamilisha
marekebisho ya Muundo wa Mamlaka na hatimaye kufanya tathmini ya
kazi (Job Evaluation and Regrading) pamoja na kurekebisha muundo
wa Mishahara.
·
Marekebisho ya
muundo wa Mamlaka yalikamilika na kuidhinishwa ndani ya kipindi
cha nusu ya kwanza ya mwaka 2004. Utakelezaji wa muundo huo
ulianza mwezi Julai 2004. Ni matumaini yangu kuwa muundo huu
mpya utasaidia kuboresha utendaji kazi na uwajibikaji ndani ya
Mamlaka.
·
kufuatia
kurekebishwa muundo, zoezi la tathmini ya kazi limeanza na
linatarajiwa kukamilika ndani ya miezi mitatu ya kwanza ya mwaka
2005.
·
Hata hivyo,
wakati tathmini ya kazi inaendelea uongozi wa Mamlaka uliofanya
hatua ya muda mfupi kwa kuongeza mishahara ya watumishi kwa
viwango vya kati ya asilimia 26 (26%) kwa kima cha juu na
asilimia 42 (42%) kwa kima cha chini.
(xii) Kuendele ana
juhudi za kuunganisha mitandao ya mawasiliano katika shughuli
zetu na kati ya viwanja, na kupevuka katika matumizi ya
teknolojia ili ituwezeshe kuboresha na kurahisisha utoaji wetu
wa huduma na pia kuongeza mapato.
·
Kazi hii bado
imeendelea kufanyika
(xiii) Kukamilisha
mkakati wa upatikanaji wa fedha za mradi wa ukarabati wa viwanja
kadhaa (11) vilivyowekewa kipaumbele maalumu.
·
Bado juhudi
zinaendelea kufanyika kwa kuwasiliana na taasisi na vyombo
mbalimbali ili kutafuta fedha za kutuwezesha kukarabati viwanja
vilivyowekewa kipaumbele maalum. Fedha za kukarabati “runway”
na Apron za DIA Terminal II zilipatikana na mradi unaanza
Januari 2005.
Ndugu Wafanyakazi wenzangu,
utekelezaji wa malengo haya ulikwenda vizuri kwa kiasi kikubwa
katika baadhi ya maeneo na vile vile maeneo mengine utekelezaji
wake haukwenda vizuri kama niliyoelezea. Aidha katika salaam
zangu za kila mwaka nimekuwa nikizungumzia mafanikio
tuliyoyapata na changamoto tulizokabiliana nazo. Tulitafakari na
kupima utendeji wetu wa kila mwaka kipekee. Ilibidi iwe hivyo
kwani “”KILA SAFARI HUANZA KWA HATUA MOJA BAADA YA
NYINGINE”
Ndugu wafanyakazi, kuzungumzia
mafanikio na mupungufu yaliyojitokeza kiutendaji ndani ya mwaka
mmoja hadi mwingine na nini tufanye kukabiliana na changamoto
hizo kumetujengea misingi ambayo inaweza kuwa vigumu kuiwekea
viwango vilivyofikiwa kwani si kila kitu hupimwa na kupata
uhalisi wake. Mafanikio yanaweza kuonekana katika uhalisi au
vinginevyo (Quantitative and Qualitative terms)
Leo tunaumaliza mwaka huu wa
2004 huku Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania ikiwa imetimiza
miaka mitano (5) tangu ilipozinduliwa rasmi tarehe 03 Desemba
1999. Basi ni vizuri kuweka mawazo yetu ndani ya miaka mitano
iliyopita ili tuone tumekua kiasi gani tukiwa tumefika nusu ya
safari yetu kuelekea kwenye DIRA tuliyojiwekea wakati Mamlaka
inaanzishwa (TAA VISION: TO BECOME A MODEL IN THE
PROVISION OF AIRPORT FACILITIES AND SERVICES IN EASTERN AFRICA
BY 2010).
Tukitazama na kutafakari kwa
ujumla wa kipindi cha miaka mitano iliyopita, ni dhahiri sote na
hata wadau watakubaliana nami kuwa utendaji kazi wa kazi zetu
umeendelea kuwa bora. Kwa mfano ndani ya kipindi hicho:
1.
Wadau wetu wemeendelea kutupongeza kwa uboreshaji huduma
zetu,
2.
pamoja na changamoto zilizotukabili, tumeendelea
kuendesha na kuhakikisha viwanja vyetu viko katika hali ya
kuruhusu ndege, abiria na mizigo kupata huduma wanazostahili,
3.
tumekuwa tukipewa pongezi na tuzo kwa ushiriki na mchango
wetu kwenye shughuli mbali mbali za kijamii na kitaifa kama vile
Janga la moto kwenye kituo cha mafuta cha TANESCO - Ubungo, Wiki
ya Taifa ya Usafirishaji na wiki ya usalama wa usafiri wa anga
na kadhalika.
4.
tarehe
17/12/2004, Taasisi iitwayo “FOUNDATION FOR EXCELLENCE IN
BUSINESS PRACTISE (FEBP)” ya Uswisi iliitunukia
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania Medali ya Dhahabu (Gold
Medal Award) kutokana na juhudi za Mamlaka za kuendeleza
uboreshaji wa huduma zake kwa msingi ya kibiashara.
Baada ya tafakari ya mwaka 2004
na kwa ufupi kabisa miaka mitano iliyopita ikiwa ni nusu ya
safari kufikia kwenye lengo kuu, naomba nitoe mwelekeo au
matarajio ya kipindi cha miaka mitano inayofuata kama ifuatavyo:
1. Tumetumia miaka
mitano iliyopita kuweka mipango mingi ya utekelezaji na kuweka
muundao unaofaa kutuwezesha kufikia malengo yetu. Pamoja na
kuendelea na kupanga ni matarajio yangu kuwa tutatumia muda
mwingi zaidi katika miaka mitano ifuatayo kwa utendaji wa yale
tuliyokwisha kupanga, hususan mipango itakayoboresha mapato na
huduma kwa kushirikisha sekta binafsi.
2. Mwelekeo muhimu pia
ni ule wa kila mtumishi kutenda kazi anayotarajiwa kutenda; kila
mmoja kwa nafasi yake; na kwa ukamilifu na muda uliopangwa. Ni
kwa jinsi hiyo tu tunaweza kuionea fahari Mamlaka yetu na kisha
kujivunia mafanikio yatakayotokana na utendaji wetu bora, na pia
kustahili kuzungumzia kuitendea haki Mamlaka kwa kuifanyia kazi
iliyokuweka ndani yake.
3.
Kuendeleza juhudi
za kukabiliana na changamoto zilizopo na zitakazojitokeza ili
kuboresha huduma zetu kwa wateja kwa kuhakikisha kuwa viwanja
vyetu ni salama katika utoaji wa huduma bora kadiri
inavyostahili.
4.
kuendelea na
ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Songwe hadi kukamilika kwake kwa
muda uliopangwa.
5.
Kuendeleza juhudi
za uimarishaji wa mapato ya Mamlaka ili kuijengea uwezo wa
kifedha.
6.
kuendeleza juhudi
za uboreshaji na upanuzi wa huduma za viwanja vya ndege kwa
kushirikisha sekta binafsi kadiri inavyowezekana.
7.
kuendeleza juhudi
za uboreshaji wa mazingira ya kazi na kujenga raslimali watu
(Human Resources) yenye uwezo wa kutoa huduma bora kwa ufanisi
zaidi.
8.
kuendeleza juhudi
za kupambana na janga la UKIMWI ambalo ni tishio kwa raslimali
watu ndani ya Mamlaka na Taifa kwa ujumla.
Malengo haya yaangaliwe katika
mtazamo wa muda mrefu (miaka mitano ijayo) na katika kipindi cha
muda muda mfupi kila idara, kiwanja au sehemu ya kazi inapaswa
kuyaainisha na kuweka mikakati ya utekelezaji. Aidha mikakati
hii ya utekelezaji ijumuishwe katika mipango ya kazi (work
plans) itakayoandaliwa.
Ndugu wafanyakazi, matarajio
haya ni baadhi tu ya mengine mengi ambayo si rahisi kuorodhesha
yote, na yanahitaji ushirikiano, juhudi na maarifa ya kila mmoja
wetu. Kwa kuzingatia hali ya ushirikiano, michango ya mawazo na
juhudi na maarifa ambayo tumekuwa nayo kwa kipindi cha miaka
mitano (5) iliyopita tangu kuanzishwa kwa Mamlaka ya Viwanja vya
Ndege Tanzania, naamini kuwa malengo yetu yatafikiwa.
Pamoja na juhudi na
ushirikiano tulionao katika utendaji wa kazi zetu ndani ya
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, sisi ni sehemu ya jamii katika
Taifa letu la Tanzania. Kwa kiasi kikubwa tunawajibika kuungana
na juhudi za kitaifa katika mapambano dhidi ya janga la
UKIMWI, umaskini na uharibifu wa mazingira.
Napenda nichukue nafasi hii kuwaomba viongozi na watumishi
wenzangu wote kwenye sehemu mbalimbali za kazi kuendelea
kuzungumzia na kuhimiza mapambano dhidi ya UKIMWI, umaskini
na uharibifu wa mazingira kama majukumu yetu ya kazi.
Mwisho, narudia tena
kuwashukuru kwa ushirikiano wenu mliouonyesha kwangu katika
utendaji wa kazi katika kipindi cha mwaka 2004 na kwa kipindi
chote cha miaka mitano iliyopita hadi kufikia hapa tulipo.
Natumaini kuwa ushirikiano huu utaimarishwa na kudumishwa zaidi
katika mwaka wa 2005.
Nawapa hongera kwa kumaliza mwaka 2004 na kuwatakia heri na
baraka katika mwaka 2005.
Ahsanteni.
Eng. P. F. H. Tesha
MKURUGENZI MKUU |